Wednesday, October 22, 2014

MAMA ALIYEPIGWA MSHALE KISA MAHARI



Ghati Bunyige akiwa amekaa kwenye benchi akisubiri huduma ya matibabu katika kituo cha afya cha Sirari wilayani Tarime mkoani Mara.
UKISTAAJABU ya Musa utayaona ya Firauni! Mwanamke mmoja, mkazi wa Kitongoji cha Buriba, Kijiji cha Sirari wilayani Tarime, Mara aitwaye Bunyige Chacha (25) amepigwa mshale kwenye makalio na mumewe, Ghati Nyamarandi kisa kikidaiwa kuanzia kwenye pesa ya mahari na watoto. Akisimulia mkasa wake mzito uliompata Oktoba 5, mwaka huu majira ya jioni, mwanamke huyo alisema siku hiyo, mumewe alirudi na kumuuliza walipo watoto wao wawili (hakuwataja majina) ambao aliwaondoa nyumbani siku kadhaa nyuma bila kumwambia.
Akasema, alipomuuliza hivyo tu, ndipo mumewe akamjia juu na kumshambulia kwa matusi huku akisema watoto aliwapeleka kuuzwa eneo linaloitwa Nyumba Ntobu. “Mume wangu alifika nyumbani, nilipomuuliza watoto wako wapi ndipo akanifungia ndani ya chumba na kunishambulia kwa matusi.
“Kwa bahati nzuri nilibahatika kutoroka na kukimbilia kwa majirani lakini wakati nikivuka uzio wa mlango nilianguka, akapata nafasi, akanirushia mshale ulionichoma sehemu ya makalio, chini ya mguu wa kulia,”alisema mwanamke huyo. 
Ghati Bunyige akiongea na mwandishi wa habari kuhusiana na mkasa aliokumbana nao. 
Mama huyo aliongeza kuwa, watoto wake wawili waliuzwa Nyumba Ntobu na baba huyo kuchukua mahari bila kumshirikisha mke suala ambalo lilizua mtafaruku ndani ya nyumba mwanamke akidai watoto wake kila siku.
“Kwanza mume wangu alimwachisha masomo binti yetu wa kwanza ambaye alikuwa akisoma darasa la tatu katika Shule ya Msingi Sirari, akamuoza Nyumba Ntobu na kupokea mahari yeye.
“Baadaye akamwachisha masomo binti yetu wa pili aliyekuwa akisoma darasa la pili katika Shule ya Msingi Nyamaraga, nchi jirani ya Kenya, akamwozesha hukohuko Nyumba Ntobu na akapokea mahari peke yake.“Baadaye nilikuja kugundua kuwa, alikuwa akipokea mahari kwa siri kwa sababu alitaka kulipia mahari ili na yeye aoe mke wa pili ambaye anaishi naye tayari, lakini ni mke wa mtu,” alisema mwanamke huyo. 
Picha ya mama huyo akiwa katika usafiri akipelekwa hospitali kwa ajili ya matibabu.
Hivi karibuni, Chama cha Waandishi wa Habari Tanzania (Tamwa) kupitia kwa mkurugenzi wake mtendaji, Valarie Msoka alifika kumwona mwanamke huyo na kumpa pole kwa tukio lililompata. Alimtaka mama huyo kumshitaki mumewe ili akamatwe na sheria ichukue mkondo wake.
Msoka amekuwa mstari wa mbele katika kupigania haki ya mama na mtoto na kulaani vitendo vinavyofanywa na jamii vya ukatili wa kijinsia kwa madai kuwa nimila au desturi za makabila husika.
Kwa upande wake, mwanasheria msaidizi wa Kata ya Sirari, Zablani Zablani aliliambia gazeti hili kuwa, mwanamke huyo alifika ofisini kwake kuomba msaada wa kisheria baada ya kujeruhiwa kwa mshale na mumewe ambapo yeye alimpeleka Kituo cha Polisi cha Sirari ili kupata PF3 na kwenda kupata matibabu katika Zahanati ya Alpha iliyopo mji mdogo wa Sirari.

No comments:

Post a Comment