Saturday, November 15, 2014

UTATA WAFUNIKA KIFO CHA NABII ELIYA, KANISA LATOA TAARIFA MAALUM

Kuanzia jana kumekuwa na post kutoka kwa watu tofauti tofauti katika mitandao ya kijamii kutokana na kifo cha aliyekuwa mwanzilishi wa kanisa la siloam nabii Eliya. moja ya post ni hapo chini. Kuna habari zinaenea kwa kasi katika mitando ya kijamii ya kwamba ,mwenye mafundisho tata ,Ndungu Munuo,aka Adamu wa Pili, Nabii Eliya, Bwana wa Majeshi, Mjumbe wa Mapenzi ya Mungu wa Kizazi cha Nne, Amefariki Dunia jana usiku, Mpaka sasa hakuna tangazo rasmi la Kanisa la Siloam. Sitofahamu hiyo inatokana na kutokuwa na taarifa za uwazi za kifo chake. kutokana na sintofahamu hiyo blog hii ilifanya mawasiliano na mmoja wa washirika wake kutaka kujua uharisia wa jambo hilo Kwa mujibu ya Mshirika niliyeongea nae amesema kuwa nabii Elia amelala na wala hajafa na hakuna kulia maana aliwaaga watu wote wakiwamo ndugu zake na familia yote na jambo hili lilikuwa linajulikana kuwa atalala na alishatafuta hadi mrithi wake ambaye ataendeleza kazi. anategemewa kulazwa mlima wa
moto (nyumbani kwake) mbezi bichi siku ya tano ya umbaji ambayo ni j2. aliongeza kusema kuwa muda wa yeye kutumika wa miaka 3 ulishaisha hivyo alishamaliza kazi. alinipa mifano kuwa manabii wengi walifanya kazi kwa miaka 3 na wakawa wamemaliza kazi yao hivyo na nabii Elia kuanzia ameanza kazi miaka 3 ilishafika ni lazima aondoke ili wengine waendelee. Mshirika huyo alikuwa anaongea kwa ujasiri na kujiamini kana kwamba alishafundishwa namna ya kujibu, kutokana na mahojiano niliyofanya nae ni kweli Nabii Eliya kafariki na maandalizi ya kumlaza nyumbani kwake zinaendelea haijafahamika kama alikuwa anaumwa au alifariki ghafla. Aliyekuwa Nabii Eliya wa kanisa la siloam shika neno trnda neno Nabii Eliya akiwa madhabahuni Wafuasi wakijipanga wakati wa yeye kuingia Kwa heri nabii Eliya


KIJANA ABUNI NDEGE MKOANI RUKWA


NOVASTUS Nkoswe ni kijana mwenye umri wa miaka 28, mkazi wa Kijiji cha Mbuluma, Kata ya Msanzi wilayani Kalambo mkoani Rukwa.
Alipopata taarifa juu ya kongamano la uwekezaji la Ukanda wa Ziwa Tanganyika lililofanyika hivi karibuni mjini Sumbawanga, mkoani Rukwa, alipata shauku ya kushiriki. Kongamano hilo lililojumuisha mikoa ya Rukwa, Katavi na Kigoma, lilifunguliwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mohammed Gharib Bilal.

Lengo kuu la kongamano hilo ilikuwa kunadi fursa nyingi za uwekezaji ambazo hazijawekezwa ipasavyo mkoani Rukwa na katika ukanda huu wa Ziwa Tanganyika. Fursa hizo ziko katika Sekta za Viwanda, Madini, Kilimo, Mifugo, Uvuvi, Afya, Elimu, Utamaduni, Michezo, Usafiri na Usafirishaji katika maeneo ya barabara, anga na majini katika Ziwa Rukwa na Tanganyika.

Nkoswe baada ya kuambiwa kwamba kwenye kongamano hilo watu binafsi na taasisi mbalimbali wanaonesha bidhaa mbalimbali zikiwemo za ubunifu, hakujali, akaona asibaki nyuma. Akaona hiyo ni fursa kwake kuonesha kipaji chake ambacho hata hivyo anasema, hakijapata uwezeshaji wa kuingia kwenye orodha ya vijana wabunifu wa vifaa vyenye manufaa kwa jamii zaidi ya kuwa fundi baiskeli maarufu kijijini kwake.

“Kuna ndugu yangu, alikuta naunda ‘ndege’ akanipa fomu akaniambia kuna maonesho ya wajasiriamali yanafanyika mjini Sumbawanga. Niliona hii ndiyo fursa na kwa bahati nikawa nimekamilisha ndege yangu, nikaanza safari ya kuja kuonesha kifaa changu hiki hapa kwenye maonesho,” anasema Nkoswe.

Akaamua kujitosa ndani ya uwanja wa Nelson Mandela Mjini Sumbawanga ambako kongamano hilo lilifanyika. Anasimulia kwamba, awali alikuwa ametengeneza pikipiki aina ya bajaj kwa kutumia mbao. Lakini baadaye akaona abadilishe muundo. Wakati anaambiwa taarifa juu ya maonesho kwenye kongamano hilo, alikuwa ametenganisha hiyo bajaj na kuanza kuunda chombo mithili ya ndege.

Kutokana na kazi yake ya ufundi baiskeli, alimudu kukusanya vyuma mbalimbali ambavyo baadhi yake, vilipatikana kutokana na shughuli yake ya ufundi baiskeli na vingine alivinunua. Alipata injini kutoka kwenye pikipiki chakavu aliyoinunua kwa mtu kijijini. Aliunda chombo hicho na kukiwekea mbawa, na vikata upepo mithili ya ndege ya kusafiria.

Kwa mujibu wake, alitumia takribani miezi miwili kuunda chombo hicho. Akakiwasha kikakubali, hatimaye akaanza safari ya kutoka kijijini kwake kwenda mjini Sumbawanga kushiriki maonesho hayo. Anasema aliweka lita nne za mafuta. Ilimchukua takribani saa 8 kutoka kijijini Mbuluma akiwa safarini.

“Niliendesha mwenyewe, njiani nilikuwa nikisimamishwa na watu mbalimbali waliokuwa wakishangaa kutokana na muundo wake,” anasema Nkoswe. Kijana huyu ambaye aliishia darasa la sita mwaka 2003 katika Shule ya Msingi Mbuluma, anasema alimudu kufika na kuingiza chombo hicho ndani ya uwanja wa maonesho. Kila aliyekikuta pembezoni mwa uwanja huo, hakuacha kushangaa.

Wakubwa kwa wadogo, walikusanyika kushangaa chombo hicho kilichotengenezwa na kufunikwa kwa karatasi za nailoni huku kikiwa na kiti kimoja cha dereva.

Anasema alianza kutengeneza chombo hicho Julai 11 mwaka huu na kumalizika ndani ya mwezi. Nkoswe ambaye anajuta kwa kutoendelea na masomo, akiwa uwanjani hapo, yeyote aliyetaka kushuhudia chombo hicho kinavyotembea, alipaswa kumpa fedha kidogo kuanzia Sh 500.

Baada ya kupokea fedha, aliingia na kuwasha chombo hicho kilichobatizwa ‘ndege ya ardhini’. Kilitembea mita kadhaa hali ambayo ilivuta watu mbalimbali wakiwemo watoto waliozunguka nacho kila kilipokwenda. “Hii hela ninayopata kutoka kwa baadhi ya watu wanaotaka kuona chombo kinavyotembea, ndiyo inanisaidia kumudu kukaa hapa mjini,” alisema Nkoswe.

Kwa mujibu wake, kufika kwake kwenye maonesho hayo, kulilenga kusaka wafadhili ambao wanaweza kuona umuhimu wa kumwendeleza. “Nina kipaji cha ufundi. Ni akili niliyozaliwa nayo. Lakini nimekuja kufikiri, kama ningeenda shule ningekuwa mbali,” anasema Nkoswe akitamani kupata wafadhili wa kumwendeleza.

Ingawa anatambua wazi kwamba chombo hicho hakiwezi kutumika kwa usafiri wa watu wengi, anaamini ubunifu na utaalamu wake wa kuunganisha vifaa kiasi cha kuwezesha kutembea barabarani, akipata wa kumwendeleza, anaweza kufanya mambo makubwa. Kijana huyu mwenye mke na watoto watatu, bado ana ndoto za kufanya mambo makubwa kupitia ufundi.

Anatamani kujiendeleza katika Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) lakini anasema kikwazo ni gharama za kujisomesha. Anasema shughuli yake kubwa ya kutengeneza baiskeli pamoja na kulima, vinamwezesha kutunza familia, ikiwemo kusomesha watoto wake wasije kuishia njiani kama ilivyokuwa kwake.

“Kama napata mtu wa kunisaidia, ningeomba nisaidiwe kupanuliwa mawazo katika ufundi hasa wa mitambo. Ningekuwa na uwezo wa kutosha, ningejiendeleza lakini sasa nikisema nikajisomeshe, hawa watoto wataishi maisha gani,” anasema. Nkoswe anatoa mwito kwa vijana hususani walioko shuleni, kukazania masomo wasije kukatisha ndoto zao za maisha. “Kwa kweli nashauri vijana, wenye nafasi ya kusoma, wasome hasa wasifanye kama mimi nilivyofanya,” anasema Nkoswe.

Katika kuelezea masikitiko ya kutoendelea na shule, anasema angekuwa na elimu ya kutosha, angeweza kubobea na kufahamika kitaifa kwa ubunifu wake. Lakini sasa, anasema anatumia akili za kawaida za kuzaliwa nazo zinazohitaji elimu ya masuala ya sayansi na teknolojia.

Anaamini kama angejiendeleza kitaaluma, angeweza kufanya maajabu kwa kutengeneza vitu ambavyo vingemletea umaarufu na kuleta manufaa kwa taifa. Ukiacha kwamba hana utaalamu, pia kutokusoma kumemnyima fursa ya kiuchumi kwani licha ya kuwa na mawazo ya kufanya mambo makuu, mtaji wake siyo mkubwa wa kufanikisha haya.

Mbali na utaalamu katika masuala ya umakenika kiasi cha kuwa maarufu kijijini kwa kutengeneza baiskeli, Nkoswe anasema kipaji kingine alicho nacho ni cha uchoraji. Anafichua siri ya kukatisha masomo ya shule ya msingi. Anasema mara nyingi, mwalimu yeyote alipoingia darasani, alikuwa na tabia ya kumchora.

Na mara nyingi, tabia hiyo iliwaudhi walimu akawa anaadhibiwa kwa viboko ambavyo ni miongoni mwa mambo yaliyomfanya akatae shule. “Sikujua kwamba shule ina umuhimu mkubwa sana katika maisha,” anasema Nkoswe. Ingawa ana ndoto za kufanya makuu akipata msaada, ana wasiwasi kutokana na kuishi kijijini ambako anaamini ni vigumu kufikiwa na mfadhili yeyote.
Hata hivyo anaomba msaada wa kuendelezwa na yeyote atakayeguswa kwa kuwasiliana naye kwa namba 0753834952.

STRABAG YATANGAZA MABADIRIKO MAKUTANO YA MOROGORO/KAWAWA KUANZIA JUMATATU

 Mkandarasi mkuu wa ujenzi wa barabara ya mabasi yaendayo haraka (BRT), Strabag International ametangaza mabadiliko ya matumizi katika makutano ya barabara za Morogoro na Kawawa.

Mabadiliko hayo yanaanza Jumatatu tarehe 17 hadi tarehe 30 mwezi huu. Akitangaza mabadiliko hayo leo jijini Dar es Salaam, Afisa uhusiano wa kampuni hiyo, Bw. Yahya Mkumba alisema mabadiliko hayo yanatokana na matengenezo yatakayokuwa yanafanyika eneo hilo.

Akielezea zaidi, alisema magari yatakayokuwa yanaelekea Ubungo kutokea Jangwani yatalazimika kutumia mchepuko uliopo kabla ya kituo cha Magomeni Mapipa kwa kuingia barabara ya mabasi yaendayo haraka.

Pia magari yatakayokuwa yanatokea Ilala Boma kuelekea Morocco, Ubungo na Jangwani yatalazimika kutumia barabara moja ya upande wa kushoto. “Wananchi watuvumilie katika kipindi hiki na tunaomba radhi kwa usumbufu wowote utakaotokea,” alisema.

Mradi wa BRT unalenga kupunguza msongamano wa magari jijini Dar es Salaam.bKilomita 20.9 za mradi huo awamu ya kwanza zipo mbioni kukamilika na kwa mujibu wa ratiba, zabuni za kupata watoa huduma zinatarajia kutangazwa mapema mwakani. Mradi huu ni moja ya miradi mikubwa duniani katika mfumo huo ambao unatarajiwa kuwa mfano katika eneo hili la Afrika ya Mashariki na kati.

Katika siku za hivi karibuni, viongozi na makundi ya watu mbalimbali yameeleza kuridhishwa  kwao na maendeleo ya mradi huo na kutoa mapendekezo ya kuuboresha zaidi.

LOWASA ATIKISA CCM NA UPINZANI

viongozi wa vyama na Serikali nchini Tanzania ambao majina yao yanatajwa na wananchi kuwa wanaweza kuwania nafasi ya urais kwenye uchaguzi mkuu mwakani.

Dar es Salaam.
Kumekucha. Pengine hilo ndilo neno linalofaa kutumika kuelezea matokeo ya utafiti kuhusu kinyang’anyiro cha urais katika Uchaguzi Mkuu 2015 ambayo yanaonyesha kuwa iwapo ungefanyika leo, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa angeibuka mshindi.

Wakati Lowassa angeibuka na ushindi kwa asilimia 13 na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda angefuatia kwa karibu akiwa na asilimia 12 huku Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa akiwa wa tatu kwa asilimia kumi na moja.


Hata hivyo, asilimia 33 ya wananchi waliohojiwa walisema bado hawajaamua wampigie kura mgombea gani.


Utafiti huo wa Taasisi ya Twaweza unayoonyesha wagombea hao kukabana kwa tofauti ya asilimia mojamoja na ambao ulitangazwa Dar es Salaam jana, ulifanywa Septemba 2014 kwa kuwahoji wananchi 1,445 kutoka Tanzania Bara.


Akitangaza matokeo hayo, mtafiti wa Twaweza, Elvis Mushi alisema utafiti huo ni wa tatu kufanyika nchini na kwamba awamu ya kwanza ilifanyika mwaka 2012 na Lowassa alipata asilimia sita kabla ya mwaka jana na mwaka huu kuibuka na asilimia 13.


Akimzungumzia Pinda, mtafiti huyo alisema mwaka 2012 alipata 16, lakini zilishuka mwaka 2013 hadi kufikia asilimia kumi na moja na kupanda tena mwaka huu hadi 12.


“Kwa upande wa Dk Slaa, mwaka 2012 na 2013 alipata asilimia 19 lakini sasa ameshuka hadi asilimia kumi na moja,” alisema Mushi.


Wagombea wengine waliotajwa na asilimia zao kwenye mabano ni Profesa Ibrahim Lipumba (6%), Dk John Magufuli (3%), Freeman Mbowe (3%), Samuel Sitta (4%), Bernard Membe (5%) na Zitto Kabwe (1%).


“Hata hivyo, kitu muhimu cha kuangalia katika ripoti hii siyo tu majina ya mgombea, bali ni idadi ya wananchi asilimia 33 ambao wamesema hawajui watamchagua nani,” aliongeza Mushi.


Ripoti hiyo inaonyesha kuwa iwapo vyama vyote vya upinzani vitaungana na kumchagua mgombea urais mmoja, asilimia 41 ya wananchi waliohojiwa walisema wangemchagua Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa, akifuatiwa na Profesa Lipumba (14%), Mbowe (11%) na Zitto Kabwe (6%).


Wanasiasa wengine waliotajwa ni Tundu Lissu, Maalim Seif Sharif Hamad, James Mbatia na Augustino Mrema ambao kila mmoja aliambulia asilimia moja.


Wengi kuchagua CCM
Pia utafiti unaeleza kuwa iwapo Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) utasimamisha mgombea mmoja wa urais dhidi ya CCM, asilimia 47 ya wananchi walisema wangeichagua CCM huku asilimia 28 wangempigia kura mgombea wa muungano wa upinzani. Asilimia 19 ya wananchi walisema watampigia kura mgombea bila kujali chama chake.


“Kura za kundi hili zitategemea ubora wa wagombea. Kama kura hizo zitagawanywa kwa CCM na upinzani, CCM itashinda urais kwa kuzidi upinzani kwa kura nyingi kiasi. Kutakuwa na kitisho kwa ushindi wa CCM endapo wapigakura wote watamchagua mtu badala ya chama watampigia mgombea wa upinzani, kitu ambacho kina uwezekano mdogo kutokea,” inasema ripoti hiyo.


Wananchi walia uchumi, afya na elimu
Wananchi walipoulizwa ni matatizo gani matatu makubwa yanayoikabili Tanzania walitaja ukosefu wa elimu bora, afya na hali mbaya ya kiuchumi na kwamba matatizo hayo yameshika nafasi ya juu kwa miaka mitatu mfululizo.


“Umaskini umeongezeka kutoka asilimia 49 mwaka 2012 hadi 63 mwaka 2014, huku matatizo ya afya yakiongezeka kutoka asilimia 40 hadi 47 na elimu imeshuka kutoka asilimia 46 mwaka jana hadi 38 mwaka huu,” alisema Mushi.


Wabunge na ahadi zao
Katika utafiti huo, imeelezwa kuwa ahadi nyingi zilizotolewa na wabunge kwenye mikutano ya kampeni wakati wa uchaguzi hazijatekelezwa na kwamba asilimia 78 ya wananchi bado wanazikumbuka.


Ahadi nyingi zilizotolewa na wagombea zilihusu miradi ya ujenzi barabara, maji, ujenzi wa hospitali, kuboresha elimu, umeme, mikopo kwa vikundi, kuongeza ajira, kujenga madaraja na kuboresha kilimo.


Pia ripoti imeweka wazi kuwa karibu nusu ya wabunge wote huenda wasirudi tena katika nyadhifa zao. Asilimia 47 ya wananchi walioulizwa iwapo watampigia tena kura mbunge wao walisema hapana huku asilimia kama hiyo wakisema ndiyo.


Akizungumzia utafiti huo, mwandishi wa habari mkongwe nchini, Jenerali Ulimwengu alihoji namna majina ya wagombea yaliyotajwa kwenye ripoti hiyo yalivyopatikana huku akipendekeza namna sahihi ya kuwalinganisha wagombea hao.


“Walitakiwa kulinganishwa kwa mfano kwenye kilimo, watuambe Mizengo Pinda anaweza kufanya nini akilinganishwa na mgombea mwingine. Vinginevyo inakuwa ni mashindano ya urembo. Tunatumia muda mrefu kumchagua mbuzi Vingunguti kumbe atachinjwa kesho,” alisema Ulimwengu.


Kwa upande wake, Dk Benson Bana wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema hatashangaa kusikia kuna watu wengine wametoa ripoti nyingine kupinga utafiti huo kwa kuwa kumekuwapo na utamaduni wa kutokukubaliana na matokeo ya namna hiyo.


“Tafiti hupingwa na tafiti, kwa hiyo mtu asianze kupinga tu, fanya kama wao (Twaweza) jifunze kutumia takwimu,” alisema huku akionyesha kukasirishwa na watu waliokuwa wakitoa maoni ya kupinga ripoti hiyo.


Kauli ya Nape
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema anakubaliana na matokeo hayo kwa kuwa yamepatikana na njia ya simu katika nchi ambayo ina watumiaji wengi wa aina hiyo ya mawasiliano.


Hata hivyo, alisema: “Tatizo ahadi nyingi zinazotolewa na viongozi kwa wananchi hazitekelezwi. Tunasema asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima lakini asilimia mbili ya viongozi ndiyo walioahidi kuhusu kilimo.”


Mjumbe wa lililokuwa Bunge la Katiba, Maria Sarungi alisema ripoti hiyo haina habari njema kwa vyama vya siasa kwa sababu inaonyesha kuwa wananchi wamekosa imani ya kupata msaada, badala yake wameanza kumtafuta ‘mkombozi’ atakayewasaidia.


“Inapotokea asimilia 41 wanasema hawajui watamchagua nani huku asilimia 10 wakisema inategemea na mtu atakayejitokeza inaonyesha wananchi wanamtafuta mtu atakayewasaidia na siyo chama.


“Mambo ya wananchi yanatatuliwa na Katiba, tatizo la utawala bora na umaskini haliletwi na vyama vya siasa linaletwa na Katiba.”MWANANCHI