Monday, October 20, 2014

LOLENA BUKWIMBA ALIZWA NA WANAFUNZI

Katika hali isiyokuwa ya kawaida na  kusikitisha mbunge wa Jimbo la Busanda mkoani Geita Lolena Bukwimba kupitia Chama cha Mapinduzi amejikuta akitoa machozi baada ya kukuta  wanafunzi wakike zaidi  25 wa shule ya sekondari Nyakamwaga wakilala chini kwa kukosa vitanda.
Hali hiyo imejitokeza jana wakati mbunge huyo  akikagua miradi ya visima 6 vya maji anavyojenga  katika kata ya Nyakamwaga wilayani Geita mkoani Geita kwa kushirikiana  na wananchi.

Mbunge huyo alipomaliza kutembelea miradi hiyo alitembelea bweni la wasichana wa shule ya sekondari Nyakamwaga na kujionea hali na adha wanayoipata watoto hao wanaolala chini na kujikuta akibubujikwa machozi.
Kufuatia hali hiyo ngumu ya maisha ya wanafunzi hao,mbunge huyo aliahidi kiasi cha shilingi milioni tano kutoka kwenye mfuko wa jimbo kwa ajili ya kununua vitanda na mahitaji mengine na kuwaomba wahisani na wafanyabishara wengine kusaidia shule hiyo.

''Jamani mimi kama mbunge wa jimbo hili nimeona hali ilivyo mbaya kwa wanafunzi wa kike wanavyoteseka  sina cha kuongea nawaomba  wahisani na wafanyabishara tuungane kusaidia jambo hili'' alisema Bukwimba

''Hatuna vitanda tunalala chini na magodoro ni machache uzio hakuna  tunaoga usiku kwa kuogopa wananchi wanaopita  hata walimu wetu  wanaishi watatu hadi wanne kwenye chumba kimoja kwa kweli tunateseka sana tunaomba tusaidiwe'' walisikika wakisema mwanafunzi hao.

Mkuu wa shule hiyo Meryciana Deusdedith alisema kuwa shule yake yenye wanafunzi 319 wakike wakiwa ni 188 na wavulana wakiwa ni 131na walimu 18 imekuwa na changamoto nyingi kama kukosa maabara na kukosa uzio jambo ambalo watoto wakike wamekuwa wakiishi kwa wasiwasi kwa kuogopa kubakwa wakati wa kuoga.

Aliongeza kuwa watoto wengi wa kike wamekuwa wakianza wengi lakini kutokana na shule hiyo kukosa mabweni ya kutosha wamekuwa hawamalizi kutokana na kurubuniwa na vijana wa mitaani kwa kuwapa mimba na kuwakimbia  na kubaki wakihangaika.

Hata hivyo alitoa shukrani zake kwa mbunge kwa kuona hilo na kuweza kusaidia kiasi hicho cha fedha na kuwaomba watu wengine kusaidia shule hiyo kwa chochote walichonacho.

No comments:

Post a Comment