Thursday, August 21, 2014

DEREVA BODABODA MBARONI KWA KUMNG’ATA MWENZAKE MDOMO NA KUONDOKA NAO


DEREVA wa bodaboda, Adinan Adam, mkazi wa Kata ya Olorieni, mkoani Arusha ametiwa
mbaroni na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumng’ata mdomo Shabani Temba na kuondoka nao.
Kijana Shabani Temba aliyepigwa na kung'twa na dereva wa bodaboda, Adinan Adam.
Akizungumza kwa uchungu wakati akitoa maelezo katika Kituo Kidogo cha Polisi cha Olorieni, Shabani alisema ameshangazwa kujikuta anapigwa kisha kung’atwa mdomo na kutolewa nyama ya mdomo pasipokuwa na kosa lolote.
Temba alisema, Alhamisi iliyopita, majira ya saa 12 jioni alifika katika kijiwe cha vyuma chakavu katika kata ya Olorieni akiwa amechoka kutokana na mizunguko yake, ndipo alipoona akae juu ya bodaboda iliyokuwa imeegeshwa kijiweni hapo huku watu wengine wakiwa pembeni yake.
“Nilipokuta pikipiki (bodaboda) hiyo ikiwa imeegeshwa katika kijiwe hicho kutokana na hali yangu ya kuchoka, niliamua kuikalia ndipo ghafla mtuhumiwa alipotokea na kuanza kunishambulia kisha kuning’ata hadi kuondoa nyama yote ya mdomo wangu,” alisema mlalamikaji huyo.
Mtuhumuiwa ambaye ni dereva wa bodaboda, Adinan Adam(aliyesimama) akiwa Kituo Kidogo cha Polisi cha Olorieni, mkoani  Arusha.
Alisema baada ya kutendewa tukio hilo, alipiga kelele hali iliyosababisha wasamaria wema waliokuwa katika eneo hilo kumkamata mtuhumiwa na kumfikisha katika kituo cha polisi ili kujibu tuhuma zinazo mkabili.
Kwa upande wake mtumuniwa huyo alipohojiwa sababu ya kutenda kosa hilo alisema ilikuwa ni hasira za kishetani kwa kuwa alifikiri kitendo cha mlalamikaji kukaa kwenye bodaboda yake kungesababisha kuibiwa.
Mtuhumiwa huyo aliomba asamehewe akidai kuwa alifanya tukio hilo kwa sababu ya hasira ambapo amebaini ni kosa baada ya kutiwa mbaroni na jeshi la polisi.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi wamelaani kitendo hicho na kudai kuwa kinaweza kuhusishwa na viashirio vya mazingira ya vitendo vya kishirikina.
“Kitendo alichofanyiwa Shabani siyo bure kitakuwa na mambo ya kishirikina, inabidi ahangaike kujua undani wake,” alisema kijana mmoja ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini.
Jeshi la polisi mkoani hapa limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba tayari limeshamkamata mtuhumiwa ambaye amefunguliwa jalada la kesi ya jinai Namba AR/RB/10937/2014 KUJERUHI.

No comments:

Post a Comment