Thursday, August 21, 2014

MGOMO MPYA WA WAFANYABIASHARA WA JIJI LA MWANZA WAANZA RASMI LEO....


Wafanyabisahara jijini Mwanza leo wameanza mgomo wa kutofungua maduka yao kwa siku zisizojulikana kwa kile walichodai Mkurugenzi wa jiji hilo, Hassan Hida amekataa kukutana nao kwa lengo la kujadili changamoto zinazowakabili.
Mgomo huo utakuwa wa pili kufanyika baada ya mara ya kwanza kutokea  wakati wafanyabiashara hao wakigomea matumizi ya  mashine za Stakabadhi za Elekitroniki (EFD).
Hata hivyo mgomo  huu  ulioanza  leo hauhusishi tena mashine za EFD badala yake umejikita katika matatizo yanayowakabili ambayo ni  ongezeko la kodi ya taka kutoka Sh 8,000 hadi 10,000, kutoza fedha za kuweka bidhaa zao nje ya duka na mambo mengine ya kukamatiwa mali zao.
 
Uamuzi huo ulifikiwa juzi katika mkutano mkuu ulioitishwa na Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania (JWT), mkoa wa Mwanza kwa lengo la kutoa taarifa za mazungumzo kati ya Serikali  juu ya matumizi ya mashine za EFD.
 
Kabla ya kufikia azimio la kutofungua maduka yao, Mwenyekiti wa JWT, mkoa wa Mwanza, Christopher Wambura aliwaeleza wafanyabiashara hao jitihada alizofanya za kukutana na mkurugenzi huyo mara zote ziligonga mwamba.
 
“Ndugu zangu wafanyabiashara mliniagiza pamoja na viongozi wenzangu tutafute suluhisho la matatizo yanayotukabili katika biashara zetu hapa jijini Mwanza, wakati tunahangaika hapa kwetu, viongozi wa kitaifa wa JWT nao walikuwa wanahangaika huko Dar es Salaam.
 
“Kwa bahati nzuri uongozi wa kitaifa umefanikiwa kwenda Ikulu na kukutana na wawakilishi wa Rais Jakaya Kikwete, baada ya hapo walikutana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda pamoja na viongozi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ndio maana leo mnaona hakuna usumbufu juu ya mashine za EFD.
 
“Wakati usumbufu wa EFD ukiwa umepotea, kero zetu zinazotukabili hapa Mwanza bado hazitaki kutatuliwa na uongozi wa jiji, mkurugenzi anatukimbia kila tunapopanga kukutana naye.
 
“Tumefanya jitihada za kukutana na Mkuu wa Mkoa, Evarist Ndikilo, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Baraka Koni na Kaimu Mkurugenzi wa Jiji, Titto Mahinya wote walionyesha jitihada za kutusaidia kukutana na mkurugenzi lakini hatukukutana mpaka leo hii,”alisema.
 
Wambura alisema pamoja na jitihada hizo, mara zote mkurugenzi amekuwa akiwaeleza kutokuwa na nafasi ya kukutana nao kwa kile alichodai kubanwa na majukumu ya kazi pamoja na kuwa nje ya mkoa kwa shughuli maalumu.
 
Pamoja na masuala mengi yaliyozungumzwa hapo, wafanyabiashara na viongozi wao walikubaliana kutofungua maduka yao hadi hapo mkurugenzi atakapokutana nao huku wakisisitiza na kutoa onyo kwa wale watakaokiuka maazimio yao.
 
Mkurugenzi anena
Mpekuzi  ilimtafuta Mkurugenzi wa jiji hilo kwa njia ya simu, ambapo alisema yupo nje ya ofisi, lakini  amewataka  viongozi  wa  JWT  wakutane  naye  kesho  saa  nne  ofisini  kwake.
 
“Nipo nje  ya  ofisi, muda huu siwezi kuzungumzia mgomo huo, lakini nimewaomba  wafungue  maduka  yao  halafu Viongozi  wao  wafike  Ofisini  kwangu  kesho  saa  nne  tuzungumze,” alisema kwa ufupi. 

TRA Mwanza
Kwa upande wa Meneja wa TRA mkoa wa Mwanza, Jeremia Lusana amesema kitendo cha  wafanyabiashara hao kugoma kinasababisha hasara kubwa katika suala la mapato huku akitishia kuwafungia lenseni za biashara zao.
 
“Tumechoka kutishwa na mgomo wa wafanyabiashara hao, umefika muda wa kuangalia namna ya kuwafungia leseni zao ili wakae nyumbani, biashara yao ina manufaa kwao na sisi, kipindi kile tulipata hasara kwa sababu mgomo ulishtukiza." Amesema  Lusana
 
Lusana amesema  TRA haina uwezo wa kuwalazimisha kufungua maduka, hivyo watasubiri hadi hapo watakapofungua ndipo watakapoendelea na shughuli zao ukusanyaji mapato kwao.

No comments:

Post a Comment