Wednesday, August 6, 2014

ZAO LA MUHOGO LAZIDI KUPATA NEEMA




ZAO la muhogo ni miongoni mwa mazao yasiyopewa kipaumbele kikubwa hapa nchini katika ulaji na kibiashara pia  huku wanasansi na watafiti wakizidi kulitangazia neema zao hilo.

Zao hilo ambalo limekumbwa na maswahibu ya magonjwa ambayo yalipelekea wakulima kukata tamaa ya kulima zao hilo limeonekana ni zao lenye manufaa kwa wakulima ikiwa watafuata maelekezo ya kilimo bora na watafiti wa kilimo

Hata hivyo imebainika kuwa zao la muhogo licha ya kwamba linalimwa kwa wingi hapa nchini lakini faida yake haijaonekana kutokana na jinsi linavyoandaliwa na kusababisha mkulima kupata faida kidogo.

Hivi sasa imebainika kuwa zao hilo ni miongoni mwa mazao yenye faida kubwa kutokana na kuonekana lina matumizi makubwa katika shughuli za viwandani ikiwa ni pamoja utengenezaji  wa sabuni ya unga, pipi, dawa, juisi  tambi,bisukuti,mafuta ya lishe,keki, kuni, mboga,nguo pamoja na bidhaa nyingine nyingi.

Hayo yalibainishwa na Bi Mariam Mtunguja ambapo alisema Tanzania inaagiza wanga (starch) kutoka nje wakati uwezekano wa kuwa na bidhaa hiyo hapa nchini ni kubwa. “ Nashangaa kuona viwanda vingi hapa Tanzania vinaagiza wanga kutoka nje ya nchi kwa bei ghali wakati uwezo wa kupata wanga kwa wingi upo kwa kutumia zao la mhogo”.


Bi Mariam Mtunguja akiendelea na kazi ndani ya maabara za MARI Dar es salaam


 Hivyo yeye kama mwanasayansi na mtafiti ameamua kuingia maabara na kufanya utafiti wa aina gani ya muhogo ambao una kiasi kikubwa na bora cha wanga ili kuwashauri wakulima na wafanyabiashara kulima zao hilo kwa manufaa yao na serikali kwa ujumla.

Alisema kuwa yeye  ameamua kufanya utafiti huo ili kupata muhogo wenye kukidhi vigezo vya wanga inayotumika viwandani ili wakulima wa zao hilo wanufaike na kilimo cha zao hilo.

“ Utafiti huu utakamilika mwezi wa tisa ambapo tayari itakuwa imefahamika ni aina gani ya muhogo inatakiwa kulimwa kwa ajili ya uzalishaji wa wanga inayohitajika viwandani” alisema Bi Mariam

Mtafiti huyo alisema kazi itabakia kwa serikali kutafuta masoko kwani anahakika wakulima wanalima mazao lakini hawana pa kuyapeleka kutokana na kutokuwa na masoko ya uhakika ya mazao yao.


Kwa habari hii ni neema kwa zao la muhogo ambalo kila ufikapo msimu wa kilimo lenyewe halifikiriwi kulimwa kama ilivyo mazao ya mahindi, mpunga Maharage na mengineyo kwani muhogo hulimwa kama zao la kuzuia njaa kutokana na uwezo wake wa kustahimili ukame hivyo wengi hulima kwa tahadhali na si kwa faida kama ilivyo kwa mazao mengine.

Hivyo kama wazalishaji wa viwandani wakiamua kukaa na wakulima wakapeana elimu ya kusindika unga wa muhogo unaotakiwa kwenye viwanda vyao, Tanzania inaweza kumaliza tatizo la njaa na umasikini kwa wakati mmoja.



Akiongea na mwandishi Bwana Athumani Idd mkulima wa mihogo katika kijiji cha Gwata mkoani Pwani alisema “serikali itutafutie soko la mihogo ili tunufaike kwani zao hili ni chanzo cha ajira kama ilivyo kwa mazao mengine”. Amesema kuwa huwa wanapata faida kiasi wakati wa mfungo wa waumini wa kiislam kwakuwa hutumia mihogo kwa ajili ya kuandaa futari vinginevyo kwao wao ni hasara tuu ila hulima kwa kuwa hawana ajira nyingine zaidi ya kilimo.

Nae Bwana Richard Kasuga afisa mawasiliano wa wizara ya kilimo na chakula alisema kuwa serikali inasubiri matokeo ya utafiti huo ili watakapo anza kutangaza bidhaa ya unga huo wawe na ukakika ya kuwa bidhaa hiyo ipo. “hatuwezi kutafuta masoko bila kuwa na uhakika wa bidhaa hiyo kuwepo,  hivyo pindi utafiti utakapokamilika watatujulisha ndipo tutukapoanza kutangaza kwa wenye viwanda na nchi zingine wanaotumia bidhaa hiyo.

 Hivi sasa zao la muhogo limezidi kupata umaarufu zaidi, ambapo  kadri siku zinavyosogea linabadilika   na kuwa zao la kibiashara hii ni kutokana na tafiti zinazoendelea kufanywa hapa nchini.

Julias James kijana anayejishughulisha na kilimo cha  mihogo mkoani Pwani alisema “tangu nizaliwe sijawahi ona zao ambalo kila sehemu ya zao ni faida kama mhogo, mzizi ni chakula, shina ni kuni wakati majani ni mboga, jamani kwani twataka kitu gani kifanyike”. Hakuishia hapo bali alizitaja faida ya kulima zao hilo ambapo alisema ni zao linalostahimili ukame na halihitaji rutuba nyingi hivyo kumpa urahisi mkulima kwa kumpunguzia gharama.

Nae mkulima wa mboga mboga katika eneo la mchicha  jijini Dar es salaam ambaye hakutaka jina lake liandikwe alisema kuwa anatamani sana kama serikali ingeruhusu wakulima wapewe mbegu mpya za mihogo kwani tangu watangaze kuwa utafiti wa kupatikana kwa mbegu mpya isioathiriwa na magonjwa umefanikiwa hatuioni madukani sasa nini faida ya kututangazia”?  aliuliza swali ambalo lilikosa mtu wa kulijibu.

Tanzania tumekuwa tukiachwa nyuma na nchi kama  kama vile Afrika  ya kusini, Nigeria,Ghana, na zingine za ulaya kama vile Italia, Thailand na kwingineko ambako kuna viwanda vikubwa kwa ajili   ya kusindika mihogo na kufanya wakulima wa nchi hizo kunufaika na kilimo hicho.

Ikumbukwe yakuwa katika kuijenga Tanizania salama bila njaa ni lazima  kanuni za kilimo bora zifuatwe, matumizi ya mbegu bora, bila kusahaku kufuata utabiri  wa hali ya hewa ili kuenenda sawa na kauli mbiu ya kilimo kwanza na si kwanza kilimo.

No comments:

Post a Comment