MWENYEKITI Mtendaji wa Makampuni ya IPP,
Dk. Reginald Mengi ni miongoni mwa wafanyabiashara wanne waliofikia
fainali ya kuwania Tuzo ya Mwaka ya Mfanyabiashara Bora Afrika (AABLA),
kundi la Afrika Mashariki.
Sherehe za tuzo za AABLA, kundi la
Afrika Mashariki zitafanyika Septemba 20 mjini Nairobi, Kenya na
zitarushwa hewani na runinga barani Afrika.
Kwa mujibu wa chaneli ya runinga ya
masuala ya fedha na biashara Afrika (CNBC Africa), ambao ndio waandaji
wa sherehe hizo, tuzo hizo za kila mwaka zimebuniwa kwa ajili ya
kutambua utendaji uliyotukuka katika biashara, wenye mafanikio makubwa
kwenye sekta zao za biashara na vile vile kwenye jamii ambako biashara
hizo zinaendeshwa.
“Tuzo hizo ni kutambua uongozi wa watu
hao katika kubadilisha sekta ya biashara kwa kuendeleza ubora wa
shughuli zao kwa kuzingatia desturi njema za kufanyabiashara na
ubunifu,”.
“CNBC Africa, inajivunia kuendeleza
utamaduni uliowekwa na tuzo hizi unaotambua na kusherekea mtazamo,
msukumo wa mafanikio na ubora mkubwa wa viongozi wafanyabiashara katika
bara la Afrika. AABLA inawatambua kipekee na kuwaheshimu viongozi ambao
wamechangia katika kuboresha uchumi wa Afrika na waelekezi wa biashara
zinazoongoza sasa,” ilisema taarifa hiyo kupitia tovuti : http://www.aabla2014.com.
Wafanyabiashara wengine watatu wateule
wa tuzo hiyo ni Ofisa Mtendaji wa Britam, Benson Wairegi, Ofisa Mtendaji
wa Centum, James Mworia, na Ofisa Mtendaji wa Crown Paints, Rakesh Rao
(Kenya).
Watanzania wengine waliyoteuliwa katika
tuzo hizo kwa makundi tofauti ni Ofisa Mtendaji wa Helvetic Solar Ltd,
Patrick Ngowi, (EA Young Business Leader), na Ofisa Mtendaji wa Techno
Brain Ltd, Manoj Shanker, (Entrepreneur of the Year).
No comments:
Post a Comment