Tuesday, August 5, 2014

ADAM MALIMA ATOA CHANGAMOTO KWA WANASAYANSI NA SERIKALI WAKATI WA UZINDUZI WA RIPOTI YA ISAAA


Tanzania imezindua ripoti ya ISAAA ya mwaka 2013 inayoonyesha matumizi ya mazao yaliyozalishwa kwa kutumia biateknolojia duniani. Uzinduzi huo uliofanyika katika ukumbi wa tume ya sayansi na teknolojia (COSTECH) jijini Dar-es salaam, ulihudhuliwa na wanasayansi, waandishi wa habari, wakuu wa asasi mbali mbali za kilimo na naibu waziri wa fedha Bwana Adam Malima ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi katika usinduzi huo.

Naibu waziri wa fedha Adam Malima (katikati) akikata utepe kuzindua ripoti ya ISAAA ya mwaka 2013


Naibu waziri Adam Malima ambaye ndiye malezi wa jukwaa la bioteknolojia kwa maendeleo ya likimo OFAB Tanzania aliwataka wanasayansi kushirikiana kwa karibu na waandishi wa habari ili kufikisha matokeo ya tafiti zao kwa jamii wanayoitumikia. “Bila sayansi na teknolojia katika kilimo tutabakia kuvuna mazao machache katika eneo kubwa kitu ambacho ni tofauti na wenzetu, kinachotakiwa ni lazima mkulima aelezwe jinsi sayansi na teknolojia inavyofanya kazi na hii ninyi wanasayansi hamuwezi ila waandishi wa habari.”

Pia aliitaka serikali na tume ya taifa ya sayansi na teknolojia kuwajali wanasayansi waliopo nchini kama ambavyo wanajaliwa sana nje ya nchi kutokana na ubora wa kazi zao kitu ambacho ni tofauti hapa nchini. Hata hivyo naibu waziri huyo katika hotuba yake alisema kuna ongezeko kubwa la watu kuliko eneo la kilimo tulilo nalo, hivyo matumizi ya bioteknolojia katika kilimo ni lazima yatumike ili kwenda sambamba na ongezeko la watu pamoja na malengo ya milenia.

Pia alisema kukataza bioteknolojia ni kumnyima fursa ya maendeleo na kuendelea kumkandamiza mkulima ambaye maisha yake hutegamea kilimo na hutumia nguvu nyingi kulima lakini mavuno ni madogo. Aliendelea kwa kuwataka wanasayansi wote nchini tafiti zao zisiishie maofisini mwao kwni wanayo kazi kubwa katika jamii ya Tanzania, wajibu wao kwa watanzania ni kuhakikisha wanapata matokeo ya tafiti zao kwa wakati, kwani hakuna maendeleo bila ya utafiti kufanyika. “Najua ya kuwa wanasayansi wengi si waongeaji, lakini waandishi wa habari wapo kwa ajili yenu, tunataka wananchi wajue matokeo ya tafiti zenu haraka iwezekanavyo hasa zinazohusu kilimo ili tuweze kutoka tulipo” alisema.

Sanjali na hayo aliwasihi waandishi wa habari kutoa elimu itakayo msaidia mkulima kuelewa ukweli na umuhimu wa teknolojia katika kilimo. “Waandishi nyie ndio mnasikika sana na kuaminiwa sana na jamii chochote mtakachokiongea mnaaminika, na ndio maana watu wengi wanawatumia nyie kwenye mambo yao hivyo basi hata katika hili pigeni kelele ili wananchi wabadirike na kufuata kanuni za kilimo bora kwa ukombozi wa mkulima.”

Shirika la Kimataifa la Huduma za Kilimo cha Kibayoteki (ISAAA) hutoa ripoti kila mwaka kuonyesha hali ya biashara ya mazao ya bayotekinolojia duniani.

Ripoti ya Mwaka 2013, ambayo tayari imezinduliwa rasmi katika nchi kadhaa Ulimwenguni inaonyesha ongezeko la wakulima wadogo wanalima mazao ya kibayoteknolojia, mapato na mafanikio kiuchumi, uhifadhi wa mazingira na mchango wa kijamii hasa kuokoa maisha ya wakulima. Ripoti hiyo inaonyesha kuwa karibu asilimia mia (100%) ya wakulima waliojaribu kulima mazao ya kibioteknolojia wanaendelea kulima mazao hayo mwaka hadi mwaka, na karibu asilimia 90 ya wakulima waliolima mazao hayo ni wakulima wadogowadogo. Matokeo hayo yanaonyesha ukuwaji wa ufahamu kuhusu teknolojia katika sekta ya kilimo.

Hata hivyo ripoti hiyo inaonyesha ukuwaji mkubwa wa uchumi kwa nchi zinazolima mazao hayo ikiwa ni nchi 27 zililima mazao hayo mwaka 2013 na kwa afrika, Afrika ya kusini imeongoza kwa kilimo hicho na nimiongoni mwa nchi 5 zinazoongoza duniani katika nchi zinazoendelea. Pia ripoti hiyo inaonyesha kuna ongezo kubwa la hekta za pamba aina ya BT cotton nchini Burkina faso na Sudani.

Mbali na hayo ripoti hiyo inaonyesha kuwa kuna majaribio ya mashambani ya pamba, mahindi na ndizi katika nchi zingine saba ambazo ni Kenya, Uganda, Cameroon, Malawi, Misri, Ghana na Nigeria wakati mradi wa mahindi yanayovumilia ukame wa WEMA unatarajiwa kukamillika kwaka 2017. Kilimo cha kibioteknolojia kimeonekana kuwa na mchango mkubwa katika maendeleo duniani kwakuwa kilimo hicho kinalimwa katika eneo dogo mazao mengi hivyo kupunguza uharibifu wa mazingira wa kukata misitu kwa ajiri ya kutafuta maeneo ya kulima. Matumizi madogo ya dawa mashambani au kutotumia kabisa dawa kitu ambacho pia husaidia utunzaji wa mazingira, kumpunguzia mkulima bajeti ya matumizi katika kilimo na kulinda viumbe hai vingine ambavyo vingeathiriwa na matumizi ya madawa hizo.

Ripoti hiyo ambayo imetolewa kwa lugha ya kiingeleza imeweka bayana maendeleo ya Afrika katika matumizi ya bioteknolojia na Afrika mashariki imeonekana kuwa katika hatua nzuri za kimaendeleo ya teknolojia hiyo ambapo Uganda na Kenya zipo katika majaribio ya shambani katika mazao ya mihogo, mahindi na ndizi na Tanzania ipo katika hatua za uchunguzi wa maabara.


Japo kuwa kumekuwa na upinzani wa matumizi ya teknolojia hiyo hapa nchini kitu ambacho kimekuwa kikiwarudisha nyuma wakulima katika kuikubali, lakini uthibitisho wa kisayansi uliotolewa na wanasayansi wenyewe pamoja na mashirika makubwa duniani kama vile CODEX Alimentarius, European Food Safety Authority (ESFA) pamoja na shirika la afya duniani (WHO) yanaonyesha kuwa tangu teknolojia hii ianze kutumika hakuna ripoti yoyote iliyotolewa kuwa teknolojia hii inamadhara kwa binadamu, wanyama wala mazingira

Hivyo basi ripoti hii iwe chachu ya maendeleo kwa wakulima Tanzania, ipo fursa iwapo kuna nia. Uwezekano wa mkulima kuwa na maendeleo makubwa ipo kama kanuni za kilimo bora zitafuatwa.

Uzinduzi wa ripoti ya ISAAA haujafanyika Tanzania pekee pia ulifanyika Afrika ya kusini, Kenya, Burkina faso, uganda ikiwa hapa Tanzania uzinduzi huo uliandaliawa na tume ya sayansi na teknolojia Tanzania (COSTECH), ISAAA kushirikiana na OFAB Tanzania,

No comments:

Post a Comment