Tuesday, October 7, 2014

HALI YA MBUNGE HIGHNESS KIWIA NI MBAYA


HALI ya Mbunge wa Ilemela, Highness Kiwia (CHADEMA), imeelezwa kuwa mbaya kutokana na kushindwa kupumua kwa kutumia pua na badala yake anatumia mdomo kitendo ambacho ni hatari.
Taarifa hiyo imetolewa jana na Kiongozi wa Operesheni Kanda ya Ziwa Magharibi, Tungaraza Njugu, wakati Baraza la Vijana CHADEMA (BAVICHA), wakitoa tamko juu ya Polisi kwa kushirikiana na Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuhatarisha amani ya nchi.
Kiwia, alisafirishwa kwenda India usiku wa Septemba 28 mwaka huu, kwa ajili ya uchunguzi zaidi na matibabu ya afya yake kutokana na matatizo ya mishipa ya kichwa.
Mbunge Kiwia, alikumbwa na tatizo hilo baada ya kushambuliwa kwa mapanga na watu wanaosadikika kuwa ni wafuasi wa CCM katika uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Kirumba jijini hapa.
Katika tukio hilo, Kiwia akiwa na mwenzake Mbunge wa Ukerewe, Salvatori Machemli (CHADEMA), inadaiwa walitekwa na kushambuliwa na wafuasi wa CCM Aprili Mosi 2012 usiku eneo la Ibanda Kirumba.
“Kutokana na nafasi aliyonayo ya ubunge, Serikali inagharamia jukumu hilo na kama chama, kimechangia kufanikisha anapata matibabu na gharama za huko ni zaidi ya dola elfu nane ambazo zitatumuika,” alisema.
Njugu, alisema vitendo vinavyofanywa na CCM vimekuwa vikihatarisha usalama wa binadamu lakini mamlaka husika imeshindwa kuchukua hatua, jambo ambalo ni ukiukwaji wa haki za binadamu, hivyo wananchi wanapaswa kutambua chama hicho kimeshindwa kusimamia na kuongoza nchi.

No comments:

Post a Comment